Monday, February 18, 2013

RAI YANGU JUU YA ELIMU


“RAI YANGU JUU YA ELIMU”

RAI yangu ni kwamba tunaweza kuifanya nchi yetu kuwa taifa kubwa, na kwamba uwezo wa kufanya hivyo umo ndani yetu. Tukiifanya nchi yetu kuwa taifa dogo ni kwa sababu tutakuwa tumejiruhusu kufanya upuuzi badala ya kufanya mambo yenye muruwa.
Wiki hii naangalia sifa moja kubwa ya taifa kubwa, sifa ambayo kila taifa kubwa lazima liwe nayo. Sifa hiyo ni mfumo wa elimu unaoandaa watu watakaokabidhiwa majukumu ya kuiendesha nchi na kuipeleka mbele. Mfumo wa elimu na maudhui yake ndilo tanuru linalooka taifa lijalo, na jinsi watoto wanavyoelimishwa ndivyo taifa linavyojengwa.
Katika jamii zetu za jadi watoto waliwekewa mfumo wa elimu uliolingana na matakwa ya jamii zetu za wakati huo. Matakwa hayo yalikuwa ni ya msingi kabisa, ambayo hayakubeba matarajio na mahitaji ya jamii ya kisasa. Jando na unyago ilikuwa ni shule ya kutosha kwa mahitaji yetu ya wakati ule.
Kijana wa kiume alifundishwa jinsi ya kufanya kazi ya ujenzi wa kaya yake, uzalishaji na ulinzi wa familia yake na jumuiya yake. Kijana wa kike alielekezwa jinsi ya kufanya kazi zake za nyumbani na jinsi ya kumfanya mume wake awe na furaha katika mapenzi. Na wote wawili walielekezwa jinsi ya kulea kizazi kilichofuata katika misingi ile ile iliyowalea wao.
Kwa jinsi hii, kila kizazi kilikirithisha kizazi kilichokirithi ujuzi, stadi na maadili yaliyotambulika kama vielelezo vya jamii husika. Kwa kuwa jamii zetu zilikuwa ni za makabila, na kwa kuwa makabila ndiyo yalikuwa mataifa yetu, elimu iliyotolewa kwa watoto na vijana ilikuwa ni ile ile kwa kabila zima. Tofauti baina ya mifumo ya elimu ndiyo iliyoeleza tofauti baina ya makabila, kwa maana haikuwezekana kuwa na mifumo ya elimu iliyotofautiana ndani ya kabila moja.
Kwa maana hiyo, basi, elimu ilikuwa ni kiungo cha jamii ndani ya jamii iliyopo, na vile vile kiungo baina ya jamii iliyopo na ile iliyoitangulia au ile inayokuja. Ni kiungo hiki kilichokuwa ‘horizontal’ na ‘vertical’ kilichoitambulisha jamii kama taifa na kilichohakikisha uendelevu wa jamii hiyo.
Vijana wa jamii yoyote waliosafiri kwenda ughaibuni walitambulika kwa elimu waliyoidhihirisha na iliyowatofautisha na vijana wengine. Elimu kwa maana hii haikuishia katika stadi za maisha na ujuzi wa kutenda mambo kama kilimo, uhunzi au uvuvi, bali pia katika tabia, adabu, heshima na haiba ya kijana. Hata safarini, mwanajamii alijitambulisha kwa haiba ya jamii yake ambayo ilitokana na elimu aliyoipata tokea utotoni.
Katika jamii za kisasa, pamoja na kwamba mambo mengi yamebadilika na tamaduni zimeingiliana na kuvurugana, bado mataifa yanahangaika kujaribu kuhifadhi angalau ile misingi inayotambulika kama mihimili ya elimu yake, ambayo inaendana na utamaduni wake. Kila taifa linalostahili kuitwa taifa linajaribu kuhifadhi zile sifa zinazolitambulisha kama taifa, tofauti na mataifa mengine, ule utamaduni unaolifanya lijitambue na litambulike kwa wengine kama taifa.
Hii ni zaidi ya kujifunza hisabati na sayansi, ni mbali zaidi ya kumiliki teknolojia ya dijitali. Ni pamoja na tabia, mwenendo, adala na haiba. Ni pamoja na jinsi ya kuingiliana na kuhusiana na watu, namna ya kuamkia na kusalimia, namna ya kuongea, namna ya kula, namna ya kujenga urafiki na uchumba.
Mshenzi mwenye shahada ya chuo kikuu hana elimu, bali ni mshenzi aliyesoma. Anao ujuzi wa mambo fulani, kama vile uwezo wa kuelezea ni malaika wangapi wanaweza kucheza ‘sindimba’ juu ya kichwa cha sindano, lakini hana elimu inayomuwezesha kuishi vyema na jirani zake. Kasoma kweli, na ana ujuzi maridhawa, lakini bado ni mshenzi. Akikualika kwake huendi, na wewe humualiki kwako.
Nieleweke kwamba nasema kwamba stadi ni sehemu ya elimu, lakini siyo elimu pekee. Inabidi iambatane na elimu ya uungwana, tabia njema na haiba yenye staha, inayojali utu, upendo, huruma, mshikamano na stahamili.
Katika mazingira yetu ya sasa tunajikuta tukiwa na changamoto kubwa katika suala zima la elimu kwa ujumla wake kwa maana kwamba tumejikwaza katika elimu ya stadi na pia tumejikwaza katika elimu ya uungwana. Kwa maana hii, tumepotea mara mbili, katika kujenga uwezo wa stadi na ufundi, na pia katika kujenga maadili ya kiungwana. Huku hatuko na huku hatuko.
Ni vigumu kusema kama nchi yetu inao mfumo wa elimu unaoweza kuelezwa kama mfumo wa taifa moja linalojenga mustakabali wake. Kila mmoja wetu anayeweza kujtengenezea mazingira ya kumsomesha (siyo kumuelimisha) mwanawe anafanya hivyo, jinsi anavyojua mwenyewe, na kwa nyenzo anazozijua mwenyewe.
Shule zinazoibuka kila mara zinakuja na mitaala yake, na mbali na mitihani ya kitaifa (kwa shule zinazochagua kuifanya) hakuna jambo linazozifanya zifanane, na kila shule inazalisha sampuli yake ya Watanzania. Ziko shule zinazozalisha Watanzania wa Kimarekani, ziko zinazozalisha Watanzania wa Kiingereza, Watanzania wa Kihindi, wa Kiarabu, wa Kifaransa, wa Kituruki, na kadhalika.
Hizo shule zinazozalisha Watanzania wasio wa Kitanzania ndizo tunazoambiwa kwamba zinafundisha vizuri masomo ya stadi. Watoto wanafundishwa hisabati na maarifa kwa viwango vya juu, na wanatafuna ung’eng’e kama wamezaliwa Oxford! Lakini watoto hao hawajui hata kuamkia wajomba zao, na baadhi ya tabia zao zinatisha.
Mbali na hawa watoto wanaotokana na familia zenye uwezo wa kuwasomesha katika shule hizo za Watanzania wasio wa Kitanzania, sasa tunakutana na wale wanaosoma katika shule za Watanzania wa Kitanzania, ambao nao ni zahma tupu.

Jenerali Ulimwengu, 13/02/2013
Gazeti la Raia Mwema

No comments: