EDUCATION/ELIMU



 
MAWAZIRI WAELEZA SHULE WANAZOSOMA WATOTO WAO
Na Abdallah Bawazir

4th March 2013

Waziri wa Nchi Ofisi ya rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wasira
Wakati umma ukiendelea kupiga kelele juu ya matokeo mabaya ya mtihani wa kidato cha nne mwaka jana, huku ikijengwa dhana kuwa viongozi waandamizi serikalini ni wa kulaumiwa kwa kuwa wamekimbizia watoto wao nje ya nchi na kwenye shule binafsi kupata elimu bora huku wakitelekeza zile za umma, baadhi ya viongozi haYo wakiwamo mawaziri wamezungumzia madai hao na kueleza wanakosoma watoto wao.

Miongoni mwa waliozungumza na NIPASHE kwa njia ya simu, wameeleza kwamba watoto wao wanasoma hapa nchini kwenye shule za serikali japokuwa kuna taarifa kwamba watoto wao wanasoma nje ya nchi na kwenye shule binafsi za gharama hapa nchini.

Baadhi  ya mawaziri waliozungumza na NIPASHE kwa nyakati tofauti  iliyowauliza kama wana watoto wao wanaosoma au waliowahi kusoma katika shule za kata wamejitetea kuwa wakati shule za Kata zinaanzishwa watoto wao walikuwa wamemaliza kusoma.

SOPHIA SIMBA
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba, alisema watoto wake hawakuwahi kusoma katika shule za kata kwa sababu wakati wanaanza kusoma hazikuwapo.

Hata hivyo, Simba alisema anao wajukuu zake ambao wanasoma katika shule za kata na kwamba wanakumbana na kero kadhaa ikiwamo kutofundishwa na walimu.

“Kimsingi watoto wangu hawajasoma katika shule za kata, lakini ninao wajukuu zangu wanaosoma shule za kata,  wanapata matatizo kweli, walimu hawafundishi,” alisema Simba.

STEVEN WASIRA

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wasira, alisema watoto wake wamesoma katika shule za sekondari za Kilakala, Tanga Ufundi na Forodhani.

Wasira alisema: “Suala la matokeo mabaya ya mtihani wa kidato cha nne hakuna haja ya kutafuta mchawi, kinachotakiwa ni kuangalia ni namna gani tutaweza kuboresha elimu yetu nchini.”

“Mimi naungana na hatua ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuunda tume, tume hii itatusaidia kujua mapungufu ni nini na namna ya kuyarekebisha, lakini tukianza kusema watoto wa mtu hawasomi katika shule za kata haitusaidii,” alisema Wasira.

Wasira aliongeza kuwa hata baadhi ya wafanyabiashara na wanasiasa watoto wao wengi hawasomi katika shule za kata, lakini hiyo haimaanishi kuwa shule za kata siyo bora.

HAWA GHASIA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia, alisema ana mtoto mmoja ambaye anasoma katika shule ya sekondari ya Mwanga ambayo inamilikiwa na Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kwa upande wake, Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, alipoulizwa kama ana watoto wanaosoma katika shule za kata alijibu kwa kifupi kuwa hawezi kujibu swali hilo kwa njia ya simu hadi afuatwe ofisini. 

WILLIAM LUKUVI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema suala la kama mawaziri wana watoto wao wanaosoma shule za sekondari za kata aulizwe Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa.

“Mimi ni Coordinator (mratibu) wa serikali siwezi kuzungumzia suala la kama mawaziri wana watoto wao wanaosoma shule za kata muulize Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi,” alisema Lukuvi.

DK. ABDALLAH KIGODA
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Kigoda, alipoulizwa kama ana watoto wake wanaosoma shule za kata au walisoma katika shule hizo alisema watoto wake wote ni wakubwa walishamaliza kusoma zamani.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Gerson Lwenge, alisema ana watoto wawili ambao walisoma shule ya sekondari ya Igwachanya ambayo ni ya kata na kwamba hivi sasa wanasoma chuo kikuu.

Lwenge alisema baadhi ya shule walimu hawafundishi. Alisema tatizo lingine ni kwamba wanafunzi hivi sasa wanasomea mitihani na walimu wanawafundisha kwa ajili ya mtihani tu.

“Kimsingi tatizo la matokeo mabaya pamoja na mambo mengine linachangiwa na wanafunzi wenyewe kusoma kwa ajili ya mtihani tu wanakuwa na mitihani ya nyuma, pia walimu hawafundishi na wanafunzi wanatumia jitihada zao kujisomea,” alisema Lwenge.

SOSPETER MUHONGO

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alisema kwa umri alionao hawezi kuwa na mtoto anayesoma katika shule za kata.

“Mimi nipo Uingereza, unaniuliza masuala ya elimu wakati ya kwangu tu yananitosha, kwanza umri wangu sina mtoto anayesoma shule za kata,” alisema Profesa Muhongo.

PROFESA MARK MWANDOSYA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Kazi maalum), Profesa Mark Mwandosya, alisema kwa sasa hana mtoto anayesoma sekondari.

Profesa Mwandosya ambaye alikuwa akizungumza na NIPASHE akiwa nje ya nchi alisema suala la kuzorota kwa elimu lisichukuliwe kisiasa, kinachotakiwa ni kujipanga upya kutafuta mbinu za kuboresha elimu nchini.

“Tukianza kutafuta mchawi tutaanza kurudi nyuma, hii ni karne ya sayansi na teknolojia, tunatakiwa tujipange ili ifikapo 2025 nchi yetu iwe ya watu wenye uelewa mzuri na kujiamini,” alisema Profesa Mwandosya.

Profesa Mwandosya alisema changamoto kubwa iliyopo ni kuboresha shule za sekondari zilizopo badala ya kuanza kuulizana mtoto wa fulani anasoma katika shule gani jambo ambalo halitasaidia.

CELINA KOMBANI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani, alisema ana watoto wanne, ambao hakuna hata mmoja aliyesoma nje ya nchi.

Alisema mwanaye wa kwanza, ambaye hakumtaja jina, alisoma hadi kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Pugu, iliyoko jijini Dar es Salaam.

Waziri Kombani alisema baadaye mwanaye huyo alisoma Shule ya Alfa (Father Pekupeku) kidato cha tano na sita, iliyoko mkoani Morogoro na kwamba, elimu ya juu alisoma katika Chuo Kikuu Mzumbe, kilichopo mkoani humo.

Alisema mwanaye wa pili, ambaye pia hakumtaja jina, alisoma sekondari ya Kizuka, iliyoko mkoani humo na kwamba, elimu ya juu alisoma katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE).

Waziri Kombani alisema mwanaye wa tatu, ambaye vilevile hakumtaja jina, alisoma kidato cha kwanza hadi sita katika Shule ya Sekondari Morogoro, wakati Shahada ya Kwanza aliipata katika Chuo Kikuu cha Tumaini na Shahada ya Pili aliipata Chuo Kikuu Mzumbe.

Alisema mwanaye wa nne, ambaye pia hakumtaja jina, hivi sasa yuko mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu Mzumbe.

“Hakuna mtoto wangu aliyesoma nje. Wakitaka wafanye uchunguzi,” alisema Kombani.

Alisema tatizo la kufaulu na kufeli, liko kwa mtoto mwenyewe na siyo shule anayosoma, licha ya shule za hapa nchini kukabiliwa na tatizo la vitendea kazi, ambavyo alisema serikali imekuwa ikilishughulikia.

GAUDENSIA KABAKA

Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka alisema watoto wote ambao hakutaja idadi yao, akiwamo wa mwisho, ambaye kwa sasa ni marehemu, walisoma katika shule za kawaida hapa nchini.

Alisema mwanaye wa kwanza, ambaye hakumtaja jina elimu ya msingi alisoma katika Shule Msingi Bunge, iliyoko jijini Dar es Salaam na kwamba, walipohamia mkoani Mwanza, aliendelea na elimu hiyo katika Shule ya Msingi Nyanza.

Alisema mwanaye huyo alisoma hadi kidato cha sita katika Shule ya Sekondari Wasichana, iliyoko mkoani Tabora na baadaye alisoma elimu ya juu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Hata hivyo, Waziri Kabaka alisema hakubaliani na dhana iliyotawala vichwani mwa watu wengi kwamba, wazazi wanaowapeleka watoto wao kusoma kwenye shule za binafsi, ni watu wenye uwezo pekee kifedha.

Alisema hata wazazi wasiokuwa na uwezo nao pia huwapeleka watoto wao kwenda kusoma kwenye shule hizo kwa kujibana kimatumizi.

“Huo utafiti mnaoufanya hautasaidia. Wazazi wanaowapeleka watoto wao (kusoma) private schools (shule za watu binafsi) siyo wenye hela tu, hata wasiokuwa na hela pia wanawapeleka,” alisema Waziri Kabaka.

BENEDICT NANGORO

Naibu Waziri  wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi,  Benedict Ole Nangoro, alisema hana watoto wanaosoma nje ya nchi.

“Hakuna mtoto wangu hata mmoja anayesoma nje ya nchi, wote wanasoma hapa nchini tena katika shule za serikali mkoani Arusha,” alisema Nangoro.

JENISTA MUHAGAMA

Mwenyekiti wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Peramiho (CCM), Jenista Muhagama, alisema watoto wake wote wanasoma katika vyuo na shule zilizopo hapa nchini.

Alisema mmoja wa watoto wake amemaliza shule ya Sekondari Matogoro iliyoko Songea na hivi sasa ni mwalimu.

Alisema katika shule hiyo pia wapo watoto wake wawili wanaoendelea na masomo ambao bado hawajamaliza.

SUZAN LYIMO
Waziri kivuli wa Elimu na Mbunge Viti Maalumu (Chadema), Suzan Lyimo, alisema watoto wake wote wanasoma katika shule za hapa nchini, mmoja anasoma shule ya Sekondari Ilboru iliyopo jijini Arusha.

Alisema wengine wawili wanasoma katika shule ya msingi Mlimani iliyopo jijini Dar es Salaam, na mwingine anasoma katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Tiba Muhimbili (Muhas).

MAGDALENA SAKAYA

Mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Tabora (CUF), Magdalena Sakaya, alisema hana mtoto yeyote anayesoma katika shule za gharama kubwa bali ana mtoto mdogo wa miaka mitano anayesoma katika shule ya misheni.

KASIMU MAJALIWA

Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi –Elimu), Kasimu Majaliwa, alisema hana imani kwamba elimu imezorota kwa sababu watoto wa viongozi wanasoma nje ya nchi na badala yake matokeo mabaya ya kidato cha nne yamesababishwa na mambo mengi. 

“Sisi tumepewa dhamana, tutahakikisha tunatekeleza kikamilifu kusimamia majukumu yetu. ziko sababu nyingi za watoto kutofanya vizuri, wapo ambao wamefeli kwa kutosoma kikamilifu, wapo waliokosa vifaa, walimu au miundombinu mibovu; siyo sababu moja tu ya kusomesha watoto nje ya nchi,” alisema.

Alisema hakuna Waziri au Mtendaji Mkuu wa Wizara ambaye anakwenda kazini na kuishia tu kusoma magazeti kwa sababu mtoto wake anakuwa anasoma nje ya nchi. 

“Tuko makini kuona elimu inapata mafanikio, ndiyo maana utaona serikali inaimarisha miundombinu, inaweka vifaa vya kufundishia na kujifunzia na kuzalisha walimu wengi kila mwaka.”

Alisema pamoja na mambo mengine, tume iliyoundwa na Waziri Mkuu itaangalia mitihani iliyopita ilivyotungwa hadi usahihishaji ili kuona kasoro na kutoa mapendekezo ya nini kifanyike.

Alisema ana watoto wawili na mmoja anasoma Ruangwa wakati mwingine bado hajaanza shule. 
Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amos Makalla, alisema matokeo mabaya ya wanafunzi katika mtihani huo yametokana na sababu nyingi zikiwamo za wanafunzi, wazazi na serikali kwa upande mwingine.

Alisema suala la kusingizia viongozi wa serikali kuwa ndiyo sababu ya kufeli kwa wanafunzi kwa kuwa hawasomeshi watoto wao kwenye shule za kata, siyo la kweli kwa kuwa wapo baadhi ya viongozi akiwamo yeye ambaye wadogo zake wawili aliowasomesha, wamemaliza katika shule za sekondari za kata huko Mtibwa.

“Kwanza ukisema viongozi wa serikali unakuwa unabagua kwa sababu utakuwa unaongelea mawaziri, makatibu wakuu na ukaacha wengine kama wabunge na wafanyakazi wengine serikalini. La msingi hapa ni kuona tulipokosea na kuparekebisha,” alisema.

Alisema suala la kufeli kwa wanafunzi linatokana na mazingira ya baadhi ya shule zenyewe kama miundombinu inayohitajika, wanafunzi na wazazi kwa upande mwingine.

Alisema kwa mfano mwanaye aliyemaliza mwaka jana na ambaye amepata daraja la nne, hakusoma katika shule za kata kwa sababu hakuchaguliwa baada ya kumaliza darasa la saba, na badala yake alimpeleka kwenye shule iliyokuwa na kila kitu; walimu, maabara na maktaba lakini bado alipata daraja la nne.

Alisema wanafunzi wengi wamefeli kutokana na kutojibidiisha katika masomo na badala yake wakatumia muda mwingi kwenye ‘facebook’ wakichati usiku kucha badala ya kusoma.
“Hapa unajiuliza mtoto huyu amepata wapi simu, moja kwa moja amepewa na mzazi wake. Kwa hiyo nasema, ni vizuri tukaboresha mazingira ya shule, tukawapa maslahi mazuri walimu, tukaweka maabara, maktaba, tukaboresha mitaala yetu, lakini pia tukawasimamia watoto wasome, kwa kuwa unaweza ukampeleka ng’ombe mtoni, lakini huwezi ukamlazimisha kunywa maji,” alisema.

Wakati mawaziri na baadhi ya wabunge wakieleza hivyo, tayari Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameunda tume maalum itakayofanya uchunguzi wa matokeo ya mtihani wa kidato cha nne ambayo yalitangazwa na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa Februari 18, mwaka huu.

Katika matokeo hayo, asilimia 60 ya wanafunzi waliofanya mtihani wa kidato cha nne Oktoba, 2012 walifeli kwa kupata daraja sifuri. 

Juzi Pinda alitangaza majina ya wajumbe tume hiyo ambao ni Mwenyekiti wa Tume ni Profesa Sifuni Mchome kutoka tume ya vyuo vikuu, Makamu mwenyekiti wa tume hiyo ni mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Bernadeta Mshashu.

Wajumbe wa tume hiyo ni pamoja na Mbunge wa Kuteuliwa na Rais, James Mbatia (NCCR Mageuzi), mbunge wa Kibiti (CCM), Abdul Marombwa, Profesa Mwajabu Possi (Profesa Mshiriki wa Elimu toka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam), Honoratha Chitanda (Makamu wa Rais Chama cha Waalimu – CWT), Daina Matemu (Katibu wa Tahossa), Juma  Mringo (Mwenyekiti Tamongsco).

Wengine ni Rajan Rakheshi, (Katibu Mtendaji Twaweza), Peter Maduki (Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii), Nurdin Mohamed, Mkuu wa Chuo cha Ualimu Alharamain, (Mjumbe toka Bakwata),  Suleiman Hemedi Khamis (Mwakilishi-Baraza la Wawakilishi), Abdallah Hemed Mohamedi (Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar), Mbarouk Jabu Makame (Baraza la Elimu Zanzibar), na Kizito Lawa, Mratibu wa Mitaala (Taasisi ya kukuza Mitaala).


CHANZO: NIPASHE


  Matokeo kidato cha IV vilio kila kona

na Sitta Tumma, Mwanza

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimetoa muda wa siku 14 Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, na Naibu wake, Philip Mulugo, kuhakikisha wamejiuzulu nyadhifa zao.
Kauli hiyo ya CHADEMA imetolewa na mwenyekiti wake taifa, Freeman Mbowe, wakati alipokuwa akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara, uliofanyika jana katika viwanja vya Furahisha Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza, ikiwa ni ufunguzi wa Baraza la Viongozi wa CHADEMA, Kanda ya Ziwa Magharibi.
Mbowe ambaye aliongoza maandamano makubwa ya magari na pikipiki kuelekea uwanjani hapo, alisema, Kawambwa, naibu wake, Mulugo, pamoja na katibu mkuu wa wizara hiyo, wameshindwa kuiongoza sekta hiyo muhimu, ndiyo maana kwa sasa wanafunzi wanaishia kuandika matusi na kupata sifuri katika mitihani ya kuingia kidato cha kwanza.
Alisema waziri huyo lazima ajiuzulu nafasi hiyo, kwani taifa ameliingiza pabaya na kuanza kuzalisha maelfu ya watoto wa maskini kumaliza elimu zao za msingi na sekondari wakiwa hawajui kusoma na kuandika.
Mbowe alisema hili ni janga la kitaifa, hivyo lazima Kawambwa aondoke ndani ya wiki mbili, vinginevyo CHADEMA itaitisha maandamano makubwa nchi nzima kushinikiza kiongozi huyo ang’oke madarakani.
“Kwa vile Kawambwa ameshindwa kuisimamia vema sekta hii ya elimu na kwa vile watoto wetu wengi wanafeli na kuishia kuandika matusi kwenye mitihani yao, CHADEMA tunampa wiki mbili awe amejiuzulu.
“Kila mwaka wanafunzi 1,200,000 hadi 1,300,000 nchi nzima wanafanya mitihani yao. Lakini wanaoshinda ni kati ya 35,000 hadi 400,000 pekee, hivyo watoto wengine wanashindwa kuendelea na masomo yao. Kwa hiyo tunataka huyu waziri na naibu wake wajiuzulu ndani ya wiki mbili,” alisema Mbowe.
Alisema, kwa sasa Tanzania inazalisha vijana wapatao 800,000 kwa mwaka ambao wanakosa fursa ya kuendelea na masomo yao na alimtaka Rais Jakaya Kikwete kuacha kucheka na kubembeleza viongozi wabovu wanaodidimiza maendeleo ya nchi na raia wake na kwamba Tanzania inakabiliwa na majanga makubwa mawili ya elimu duni na udini.
Kuhusu Bunge kutoonyeshwa ‘live’, Mbowe alimuonya Spika Anna Makinda na wasaidizi wake kuacha kutumia madaraka yao kuwanyima uhuru na haki wananchi na kwamba Watanzania wanahitaji kuwaona wabunge wao wabovu na wazuri ili mwaka 2015 wafanye maamuzi magumu ya kutokuwachagua au kuwachagua tena.
“Makinda tumemwambia aache ubabaishaji katika uendeshaji wa Bunge. Watanzania wanataka kuwaona wabunge wao wanaolala na wanaoshangilia hoja za hovyo! Tunataka Bunge liendeshwe kwa mazingira yanayomwezesha mwananchi kufahamu kila kitu kinachojadiliwa katika chombo hicho.
Akizungumzia maamuzi ya CHADEMA kuanzisha uongozi wa kikanda, Mbowe ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Hai, alisema sera ya majimbo ni nguzo kubwa katika kuleta maendeleo kwa wananchi, hivyo chama chake hakijakosea kufanya hivyo na wanahitaji Tanzania igawanywe katika uongozi kwa ngazi ya majimbo ili kurahisisha upatikanaji wa maendeleo.
Alisema licha ya kwamba sera yao hiyo inabezwa na CCM, lakini ndiyo mkombozi mkubwa katika adha ya umaskini miongoni mwa wananchi, hivyo wataisimamia kikamilifu kuanzia sasa na baada ya kuingia Ikulu katika uchaguzi mkuu ujao mwaka 2015.
Mbowe aliishutumu CCM na viongozi wake kwa kueneza siasa mbaya za udini, kwani walianza kuishambulia CUF kwa madai kwamba ni chama cha Kiislamu na baadaye CHADEMA kwamba ni chama cha Wakristo, jambo ambalo kwa sasa limejaa mbegu mbaya ya kuwepo kwa mzozo wa kidini na aliwataka Watanzania kutokubali kugawanywa kwa ukabila, udini na ukanda na wasiichague CCM 2015.
Mbali ya kauli ya Mbowe, matokeo hayo ya kidato cha nne yamelalamikiwa kila kona nchini.
Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, James Mbatia, amemtaka Rais Jakaya Kikwete, kutangaza tatizo la elimu kuwa janga la kitaifa na kumtimua Waziri Kawambwa.
Mbali na Mbatia wadau mbalimbali na wananchi nao wametaka Rais Kikwete kuivunja Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na kuisuka upya.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mbatia alisema kuanguka kwa elimu kumetokana na CCM kuendekeza mambo ya ushabiki wa kisiasa hata kwenye mambo yanayolihusu taifa.
Mbatia alieleza kuwa mitaala ndio dira ya elimu lakini akashangazwa na serikali kutokuwa na mitaala rasmi na hata alipolieleza Bunge jambo hilo, wabunge wa CCM walimjia juu na kuamua kuizima hoja hiyo.
“Serikali haijawahi kuwa na mitaala rasmi, taifa halina dira ya elimu; kuna mkanganyiko katika vitabu na ufisadi uliopo unaliangusha taifa hakuna mfumo bali waziri anafanya anavyoamua,” alisema.
Alirejea hoja yake kuwa Chama cha Mapinduzi (CCM), kimejiaibisha kukataa hoja yake na kueleza kuwa watoto wengi waliofeli ni wa CCM.
“CCM ndiyo ina majimbo mengi kwa hiyo waliofeli ni watoto wao; sasa badala ya kuhakikisha inaondoa kirusi katika elimu yenyewe inaingiza itikadi za vyama katika suala la elimu.”
Aidha alitaka vitabu vinavyotumika sasa mashuleni, vizuiwe na bajeti ijayo vipengere kumi muhimu iwe ni elimu ili kunusuru anguko la sekta hiyo kwani wizara iliyopo haiwezi kuyatatua peke yake.
Kwa upande wake, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimesema kauli ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Shukuru Kawambwa, kuwa matokeo hayo yameisikitisha serikali haitakuwa na maana yoyote kama haitakuwa na jitihada za makusudi kuikwamua elimu ya Tanzania kutoka katika mfumo uliopo sasa, Waziri Kivuli wa Wizara ya Elimu na Mafaunzo ya Ufundi, Suzan Lyimo, alisema serikali imekuwa ikidharau kutatua matatizo ya msingi inayoikabili sekta ya elimu.
Alitaja moja ya matatizo ya walimu ni mazingira mabovu ya kufundishia, hali inayowafanya wengi wao wasiwe na ari ya kufanya kazi hiyo.
“Serikali imeisusa sekta ya elimu na hii ni kwa sababu viongozi wa serikali hawawasomeshi watoto wao katika shule za serikali hivyo hawana uchungu na matatizo yanayowakabili walimu na wanafunzi wa shule hizo,” alisema Lyimo.
Aliongeza kuwa hata katika masuala ya ukaguzi wa maendeleo ya elimu kama ilivyokuwa zamani kwa sasa hautiliwi mkazo kutokana na bajeti finyu.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe, alimtaka Waziri wa Elimu, Mafunzo ya Ufundi, Shukuru Kawambwa na Naibu wake, Phillipo Mulugo, kuwajibika na kupisha katika wizara hiyo.
Pia alimtaka Rais Kikwete aichukue wizara hiyo na kuwa chini ya ofisi yake.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Zitto alisema kuwa ni muhimu viongozi wanaosimamia wizara hiyo wakawajibika.
Alisema uwajibikaji huo unapaswa kufanyika kuanzia kwa katibu mkuu wa wizara hiyo pamoja na kamishna.
“Najua kuwa haina uhusiano wa moja kwa moja maana matatizo ya elimu ni makubwa sana nchini. Lakini ni lazima kitu fulani kitokee ili kufanya mabadiliko. Uwajibikaji ni njia mojawapo inayoleta nidhamu na uharaka katika utendaji kazi, alisema na kuongeza: “…namna hii (zaidi ya nusu ya wahitimu kupata sifuri) na takriban asilimia 90 kufeli kwa kupata daraja la nne na daraja la sifuri ni mwaka wa tatu sasa mfululizo. Matokeo yakitoka tunasema weeee mpaka povu linatoka.
“Baada ya wiki tumeshasahau na hakuna hatua yoyote. Lazima uwajibikaji utokee,” alisema Zitto.
Alisema ni muhimu Rais Kikwete aichukue Wizara ya Elimu, yaani Waziri wa Elimu awe yeye, pia kuwe na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Elimu.
Zitto alisema kuwa Rais anapaswa aelezwe kuwa iwapo matokeo yatabaki hivi mwakani na yeye atatakiwa kuondoka katika nafasi hiyo.
“Najua wa mwakani ndio wako kidato cha nne sasa na wana msingi mbaya tayari lakini sio jukumu letu kujipa majibu bali ni jukumu letu kuiambia serikali; hapana! Tuwape masharti. Vinginevyo haya yatakwisha na mwakani itakuja,” alisema.
Zitto alisema elimu iliyopo sasa inazalisha matabaka ndani ya jamii na ni hatari kwa uhai wa taifa.
Mbali ya maoni hayo, wadau wengine walimtaka waziri mwenye dhamana ajiuzulu.
Mmoja wa wadau hao Selemani Juma, alisema kadri siku zinavyokwenda ndivyo anguko la elimu linavyozidi kuwa kubwa.
Alisema mvurugano uliopo katika matumizi ya vitabu na kuacha vitabu vilivyokuwa vinatumika na kuanza kutumia vitabu vingine ambavyo alidai vipo kwa ajili ya maslahi ya viongozi, havina ubora na viwango vya kufundishia.
Naye Janeth Alphonce, alieleza kuwa wizara husika chini ya Dk. Kawambwa, haiwezi kutatua mifumo ya elimu ambayo ni ya miaka mingi na haiendani na soko la elimu ya sasa.
Mwalimu John Bosco Katatumba alisema matokeo hayo ni tafsiri ya hali ya ubovu wa elimu nchini katika kipindi cha miaka 10 iliyopita.
Akitoa maoni kwa njia ya simu, Lucas Nyangaramila (61), mkazi wa Arusha alisema chanzo cha wanafunzi kufanya vibaya ni mitaala ya elimu mibovu kwani kila baada ya muda imekuwa ikibadilishwa.
“Mwanafunzi aliyesoma kwa lugha ya Kiswahili kuanzia darasa la kwanza hadi la saba na kusoma Kiingereza awapo sekondari ni vugumu kwake kuelewa lugha ya Kiingereza mapema na badala yake kuongozwa na wale waliosoma shule za Kiingereza kuanzia shule za msingi,” alisema.
Naye Thobiace Boniface mkazi wa Mbezi Beach jijijini Dar es Salaam, alisema matokeo ni mabaya na yanatia aibu na aliiomba serikali ifute shule za kata kwa sababu ya maandalizi duni.
Hali kadhalika, Mama Saidi mkazi wa Mabibo alisema kukua kwa sayansi na teknolojia kumechangia kwa kiasi kikubwa kwa elimu ya wanafunzi kushuka hapa nchini.
“Hii mitandao kama vile intaneti, facebook, twitter n.k bila kusahau simu za mikononi imekuwa ni kikwazo cha elimu kwa watoto wetu kwani wamekuwa wakitumia muda mwingi kuwasiliana na watu mbalimbali kwenye mitando hiyo, sasa muda wa kujisomea utatoka wapi?” alihoji.
Kwa upande wake David Mlay, alisema kitendo cha shule za serikali kutofanya vizuri hata kwa shule zake za vipaji maalumu ambazo ndizo zilikuwa tegemeo, ni anguko kubwa la elimu nchini.


Chanzo: Tanzania Daima: jumatano, 20 februari 2013



“RAI YANGU JUU YA ELIMU”
RAI yangu ni kwamba tunaweza kuifanya nchi yetu kuwa taifa kubwa, na kwamba uwezo wa kufanya hivyo umo ndani yetu. Tukiifanya nchi yetu kuwa taifa dogo ni kwa sababu tutakuwa tumejiruhusu kufanya upuuzi badala ya kufanya mambo yenye muruwa.
Wiki hii naangalia sifa moja kubwa ya taifa kubwa, sifa ambayo kila taifa kubwa lazima liwe nayo. Sifa hiyo ni mfumo wa elimu unaoandaa watu watakaokabidhiwa majukumu ya kuiendesha nchi na kuipeleka mbele. Mfumo wa elimu na maudhui yake ndilo tanuru linalooka taifa lijalo, na jinsi watoto wanavyoelimishwa ndivyo taifa linavyojengwa.
Katika jamii zetu za jadi watoto waliwekewa mfumo wa elimu uliolingana na matakwa ya jamii zetu za wakati huo. Matakwa hayo yalikuwa ni ya msingi kabisa, ambayo hayakubeba matarajio na mahitaji ya jamii ya kisasa. Jando na unyago ilikuwa ni shule ya kutosha kwa mahitaji yetu ya wakati ule.
Kijana wa kiume alifundishwa jinsi ya kufanya kazi ya ujenzi wa kaya yake, uzalishaji na ulinzi wa familia yake na jumuiya yake. Kijana wa kike alielekezwa jinsi ya kufanya kazi zake za nyumbani na jinsi ya kumfanya mume wake awe na furaha katika mapenzi. Na wote wawili walielekezwa jinsi ya kulea kizazi kilichofuata katika misingi ile ile iliyowalea wao.
Kwa jinsi hii, kila kizazi kilikirithisha kizazi kilichokirithi ujuzi, stadi na maadili yaliyotambulika kama vielelezo vya jamii husika. Kwa kuwa jamii zetu zilikuwa ni za makabila, na kwa kuwa makabila ndiyo yalikuwa mataifa yetu, elimu iliyotolewa kwa watoto na vijana ilikuwa ni ile ile kwa kabila zima. Tofauti baina ya mifumo ya elimu ndiyo iliyoeleza tofauti baina ya makabila, kwa maana haikuwezekana kuwa na mifumo ya elimu iliyotofautiana ndani ya kabila moja.
Kwa maana hiyo, basi, elimu ilikuwa ni kiungo cha jamii ndani ya jamii iliyopo, na vile vile kiungo baina ya jamii iliyopo na ile iliyoitangulia au ile inayokuja. Ni kiungo hiki kilichokuwa ‘horizontal’ na ‘vertical’ kilichoitambulisha jamii kama taifa na kilichohakikisha uendelevu wa jamii hiyo.
Vijana wa jamii yoyote waliosafiri kwenda ughaibuni walitambulika kwa elimu waliyoidhihirisha na iliyowatofautisha na vijana wengine. Elimu kwa maana hii haikuishia katika stadi za maisha na ujuzi wa kutenda mambo kama kilimo, uhunzi au uvuvi, bali pia katika tabia, adabu, heshima na haiba ya kijana. Hata safarini, mwanajamii alijitambulisha kwa haiba ya jamii yake ambayo ilitokana na elimu aliyoipata tokea utotoni.
Katika jamii za kisasa, pamoja na kwamba mambo mengi yamebadilika na tamaduni zimeingiliana na kuvurugana, bado mataifa yanahangaika kujaribu kuhifadhi angalau ile misingi inayotambulika kama mihimili ya elimu yake, ambayo inaendana na utamaduni wake. Kila taifa linalostahili kuitwa taifa linajaribu kuhifadhi zile sifa zinazolitambulisha kama taifa, tofauti na mataifa mengine, ule utamaduni unaolifanya lijitambue na litambulike kwa wengine kama taifa.
Hii ni zaidi ya kujifunza hisabati na sayansi, ni mbali zaidi ya kumiliki teknolojia ya dijitali. Ni pamoja na tabia, mwenendo, adala na haiba. Ni pamoja na jinsi ya kuingiliana na kuhusiana na watu, namna ya kuamkia na kusalimia, namna ya kuongea, namna ya kula, namna ya kujenga urafiki na uchumba.
Mshenzi mwenye shahada ya chuo kikuu hana elimu, bali ni mshenzi aliyesoma. Anao ujuzi wa mambo fulani, kama vile uwezo wa kuelezea ni malaika wangapi wanaweza kucheza ‘sindimba’ juu ya kichwa cha sindano, lakini hana elimu inayomuwezesha kuishi vyema na jirani zake. Kasoma kweli, na ana ujuzi maridhawa, lakini bado ni mshenzi. Akikualika kwake huendi, na wewe humualiki kwako.
Nieleweke kwamba nasema kwamba stadi ni sehemu ya elimu, lakini siyo elimu pekee. Inabidi iambatane na elimu ya uungwana, tabia njema na haiba yenye staha, inayojali utu, upendo, huruma, mshikamano na stahamili.
Katika mazingira yetu ya sasa tunajikuta tukiwa na changamoto kubwa katika suala zima la elimu kwa ujumla wake kwa maana kwamba tumejikwaza katika elimu ya stadi na pia tumejikwaza katika elimu ya uungwana. Kwa maana hii, tumepotea mara mbili, katika kujenga uwezo wa stadi na ufundi, na pia katika kujenga maadili ya kiungwana. Huku hatuko na huku hatuko.
Ni vigumu kusema kama nchi yetu inao mfumo wa elimu unaoweza kuelezwa kama mfumo wa taifa moja linalojenga mustakabali wake. Kila mmoja wetu anayeweza kujtengenezea mazingira ya kumsomesha (siyo kumuelimisha) mwanawe anafanya hivyo, jinsi anavyojua mwenyewe, na kwa nyenzo anazozijua mwenyewe.
Shule zinazoibuka kila mara zinakuja na mitaala yake, na mbali na mitihani ya kitaifa (kwa shule zinazochagua kuifanya) hakuna jambo linazozifanya zifanane, na kila shule inazalisha sampuli yake ya Watanzania. Ziko shule zinazozalisha Watanzania wa Kimarekani, ziko zinazozalisha Watanzania wa Kiingereza, Watanzania wa Kihindi, wa Kiarabu, wa Kifaransa, wa Kituruki, na kadhalika.
Hizo shule zinazozalisha Watanzania wasio wa Kitanzania ndizo tunazoambiwa kwamba zinafundisha vizuri masomo ya stadi. Watoto wanafundishwa hisabati na maarifa kwa viwango vya juu, na wanatafuna ung’eng’e kama wamezaliwa Oxford! Lakini watoto hao hawajui hata kuamkia wajomba zao, na baadhi ya tabia zao zinatisha.
Mbali na hawa watoto wanaotokana na familia zenye uwezo wa kuwasomesha katika shule hizo za Watanzania wasio wa Kitanzania, sasa tunakutana na wale wanaosoma katika shule za Watanzania wa Kitanzania, ambao nao ni zahma tupu.

Jenerali Ulimwengu, 13/02/2013
Gazeti la Raia Mwema

No comments: