Sunday, February 3, 2013


TULAANI UBAKAJI, ULAWITI, UPORAJI WANAFUNZI VYUO VIKUU

WIKI mbili zilizopita kumekuwa na taarifa za aibu na za kusikitisha kutokana na mfululizo wa matukio ya ubakaji, ulawiti na uporaji wa vifaa vya wanafunzi wanaosoma katika vyuo vikuu mbalimbali hapa nchini unaoendelea.
Licha ya kwamba ubakaji umekithiri kwa kiasi kikubwa hapa nchini na hauripotiwi ipasavyo kwenye vyombo vya habari au jamii hairipoti, lakini haya yanatutia doa.
Kuna matukio kama haya yanawatokea wanajamii huko vijijini, au makundi yaliyoko pembezoni na hawawezi kupaza sauti au kuandamana kama wanavyofanya wanafunzi wa vyuo vikuu. Maandamano haya ni alama ya jinsi ambavyo hali ni mbaya huko vijijini na wananchi walio wengi wameshateswa na kuumizwa.
Pamoja na matukio haya ya udhalilishaji wa kijinsia, ya kubakwa kwa wasichana na kulawitiwa kwa wavulana, kumeendelea kuwepo kwa matukio ya mauaji ya kinyama kama hili la mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha St. John’s cha Dodoma, lililotokea Januari 20, mwaka huu kwa kubakwa na kuuawa.
Tunajiuliza haki ya raia kuishi iko wapi? Kwanini waliofanya unyama huu hadi sasa hawajakamatwa na kuchukuliwa hatua? Je, sheria ya adhabu ya makosa ya kujamiiana (SOSPA) ya mwaka 1998 imefia wapi? Je, masikini au mwananchi wa kawaida akiuawa hana thamani?
Tukio hili limetanguliwa na matukio kadhaa yaliyoripotiwa mwaka jana na kusababisha wanafunzi wa chuo hicho kuandamana hadi Kituo cha Polisi, Mei 30 mwaka jana, ambayo ni ubakaji, ulawiti na uporaji wa vifaa kama simu, laptop, Tv na redio.
Tunasikitika kuwa hadi leo Jeshi la Polisi halijachukua hatua za kudhibiti matukio hayo.
Mwaka 2007 nikiwa Chuo Kikuu cha Mt. Augustine Mwanza, tuliokuwa tukiishi Malimbe, Nganza, Swea, Mkolani na Nyegezi Corner matukio kama haya yalikuwepo na tuliandamana hadi kwa Mkuu wa Mkoa wakati huo Dk. Alex Msekela, lakini madai yetu hakuyafanyia kazi.Tukio hili limeendelea hadi Dar es Salaam, na kusababisha wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) wanaoishi Kigamboni wilayani Temeke, kuandamana kudai ulinzi baada ya wenzao kubakwa, kulawitiwa na kuporwa vifaa na mali.
Mwaka jana matukio kama haya yameripotiwa katika vyuo vikuu vya Mt. Augustine (SAUT) Mwanza, RUCO Iringa, na St John’s Dodoma, lakini hakuna hatua za haraka za kukomesha matukio haya zimechukuliwa. Wanafunzi wanaoishi nje ya mabweni (Hosteli) ya vyuo vikuu wamekuwa waathirika wa tatizo la wizi au uporaji.
Matukio ya ubakaji na ulawiti na udhalilishaji wa kijinsia yameendelea kwa muda mrefu.
Utafiti wa TAMWA uliofanyika mwaka jana katika visiwa vya Pemba na Unguja umebaini kuwa mwaka 2012 pekee kulikuwa na matukio 400 ya ubakaji, wakati Mkoa wa Kilimanjaro pekee ulikuwa na kesi 46 za ubakaji zilizoripotiwa polisi.
Lakini hatuchunguzi kwa kina wanawake, wasichana, vikongwe, na watoto masikini walioko vijijini ambao wanabakwa usiku na mchana na habari zao hazitangazwi.
Jamii nzima tuungane kulaani matukio haya yanayoendelea, tuwalaani viongozi waliotakiwa kuchukua hatua za kulimaliza tatizo hili na hawafanyi hivyo.
Jamii ikatae unyanyasaji, na kukumbatiwa kwa wahuni au wahalifu wa aina hii ambao wanatuharibia taifa letu.
Tunajua kuwa kitendo cha udhalilishaji kijinsia kinaathiri kisaikolojia na kama wasomi wanabakwa, tunadidimiza nguvu kazi ya taifa hili.
Je, kama tunakuwa na wasomi waliochanganyikiwa kwa kuumizwa kisaikolojia tunaandaa taifa gani? Si kwamba ni mwanzo wa kuwa masikini zaidi?
Kutokana na matukio haya ya aibu ambayo yanalidhalilisha taifa letu, sisi kama wanajamii tunapaswa kulaani na kulitaka Jeshi la Polisi kuwawajibisha viongozi na wakuu wa vituo ambao wamepokea malalamiko ya wanafunzi wa vyuo vikuu, Kigambani na Dodoma na hawakuchukua hatua.
Pia Jeshi la Polisi liache kupuuza madai ya wananchi juu ya wizi unaotokea na kufanya kazi yake ya kulinda raia na mali zao.
Jeshi la Polisi liache kutumia nguvu kubwa kuwasambaratisha wananchi wanaodai haki badala yake nguvu zitumike kuwalinda kama ilivyofanyika Kigamboni juzi.
Inashangaza kuona wanafunzi wanadai ulinzi wa askari watatu wananyimwa, lakini wakiandamana, askari 500 wanapelekwa kuwapiga mabomu.
Uongozi wa serikali za mitaa na vijiji ambao matukio hayo yanafanyika, wawajibike kwa kushindwa kusimamia kikamilifu ulinzi wa raia na mali zao, na serikali kuu ihakikishe inaboresha mazingira ya ulinzi, upatikanaji wa vituo vya polisi na vitendea kazi katika mazingira hatarishi hasa wanakoishi wanafunzi.
Tuchukue hatua haraka inavyowezekana kudhibiti matukio haya, na sote tuseme ‘hapana ubakaji kwa Watanzania wote!’

Deogratius Temba Mwananchi: jumapili, 27 januari 2013

No comments: