Friday, January 11, 2013


‘WAZAZI KIKWAZO KUPOROMOKA MAADILI YA WATOTO’

na Danson Kaijage, Dodoma


UZEMBE wa wazazi na walezi kushindwa kuwalea watoto wao katika misingi bora ya kimaadili umeelezwa kusababisha kuporomoka kwa maadili ya watoto nchini.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Mkuu wa Wilaya ya Bahi, Betty Mkwasa alipokuwa akizungumza na wazazi wa watoto wa shule ya msingi ya St. Ignatius katika mahafali ya tatu ya darasa la saba katika shule hiyo.
Alisema kuwa hivi sasa wazazi wamekuwa wakilalamika kwa madai kuwa watoto wengi wamepoteza maadili ya Mtanzania lakini wazazi hao na walezi wamesahau kuwa hawana muda wa kuzungumza nao.
Aliongeza kuwa wazazi wengi wamejijengea tabia ya kuwapeleka watoto wao katika shule za bweni kuanzia shule ya chekechea jambo ambalo linawanyima fursa ya kukaa na wazazi wao.
“Mimi nashangaa yaani wazazi wengi wanawapeleka watoto wao katika shule hizi za bweni mtoto akiwa mdogo kabisa kuanzia chekechea hadi Chuo Kikuu, sasa kwa hali hiyo unafikiria mtoto ataweza kujua hata mila za familia husika kweli.
“Yaani wazazi wamegeuza walimu kama ni wazazi kamili wa watoto, wazazi wengi hawana  muda kabisa wa kukaa na watoto wao wakawasikiliza kujua wana mawazo gani, matokeo yake watoto wanakuwa na tabia zao na hawana uelewa juu ya mila na desturi husika za familia au kabila,”  alisema.
Aliwataka wazazi kuwa karibu na walimu ili kuweza kubaini matatizo ambayo yanaweza kujitokeza pindi watoto wawapo shuleni ikiwemo kujua maendeleo ya mtoto wake.

jumatatu, 20 agosti 2012, Tanzania Daima

No comments: