Sunday, March 17, 2013


WANAUME NENDENI KLINIKI MTAMBUA AFYA ZA WAKE ZENU`
Na Mwandishi wetu
17th March 2013

Wanaume wameshauriwa kushiriki kliniki ili waweze kutambua afya za wake zao wanapokuwa wajawazito badala ya kuwatelekeza.
Ushauri huo ulitolewa jana na Meya wa manispaa ya Dodoma, Emanuel Mwiliko, wakati alipokua akifungua kambi ya kupima afya kwa akina mama na watoto mjini hapa.
Mwiliko alisema kuwa kumekuwapo na tatizo kubwa kwa wanaume wengi nchini kuwa wazito kwenda kliniki hali inayosababisha wasiweze kujua afya za wake zao wanapokuwa na matatizo.
Alisema kuwa ifike wakati wanaume wabadilike kutoka katika mtazamo walio nao hivi sasa na kuanza kushiriki kuwapeleka wake zao kliniki ili waweze kuzitambua afya za wenzi wao.
“Sisi akina baba tumekuwa mstari wa nyuma katika kushiriki kliniki hivyo natoa wito tujitokeze katika kushiriki kliniki sisi na wake zetu hali ambayo itatusaidia kujua afya zao zinaendeleaje,” alisema Mwiliko.
Aidha alitoa wito kwa jamii kuwa karibu na akina mama wajawazito ili kuhahakisha kuwa wanajifungua salama.
“Tuhahakishe kuwa tunafuatilia afya za akinamama wajawazito kabla na baada ya kujifunga ili kuweza kuwasaidia katika kuwalea watoto wao katika afya iliyo njema,” alisema.
Naye meneja wa hospitali ya Agha khan mkoani hapa ambao wameandaa kambi hiyo ya kupima afya bila malipo kwa wananchi, Kibe Abel, alisema kuwa lengo ni kuwasogezea wananchi huduma karibu.
Abel alisema kuwa huduma hizo zinatolewa kupitia mradi wa tuunganishe mikono katika kuboresha afya ya mama na mtoto (JHI) kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Canada (CIDA).
“Huduma tunazo zitoa ni kupima watoto na akimama wajawazito pamoja na kutoa elimu jinsi gani akina mama wanaweza kunyonyesha na namna ya kuwalea watoto wao katika afya nzuri,” alisema Abel.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments: